Tuesday 3 June 2014

Lissu alia na maghembe kwa kulipendelea jimbo lake

MBUNGE wa Singida Mashariki, Tundu Lissu MBUNGE wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA), ameilaumu serikali kwa kutoa fedha za miradi ya maji kwa kupendelea baadhi ya maeneo wanayotoka viongozi.
Lissu, alitoa lawama hizo jana bungeni alipokuwa akichangia bajeti ya Wizara ya Maji, kwa mwaka 2014/2015 iliyowasilishwa na Profesa Jumanne Maghembe.
Alisema mgawo wa fedha hizo unaonyesha kuwa mikoa yenye  vyanzo vya uhakika na nafuu ya maji, imetengewa fedha nyingi kuliko mikoa yenye hali mbaya na isiyo na vyanzo vya maji.
Akitolea mfano, Lissu alisema mikoa yenye hali mbaya kama Dodoma, Singida, Shinyanga, Shimiyu imetengewa fedha ndogo ukilinganisha na mikoa yenye nafuu ya maji kama Tanga, Kilimanjaro, Mtwara na Mbeya.
Alisema mgawanyo wa fedha za miradi ya maji umefanywa kwa upendeleo kwani maeneo ya mawaziri yametengewa fedha nyingi kuliko maeneo ya wabunge.
“Mwaka huu, Mkoa wa Dodoma, umetengewa sh bilioni 7, Singida sh bilioni 3, Shinynga sh bilioni 3, Simiyu bilioni 5, lakini mikoa yenye nafuu ya maji kama Tanga sh bilioni 10, Kilimanjaro bilioni sita, Mbeya sh bilioni tisa, Mtwara bilioni saba.
“Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mwanga anayotoka Waziri Maghembe peke yake imetengewa sh bilioni 1.5, wilaya ya Makete anayotoka aliyekuwa Naibu wako Binilith Mahenge, imetengewa bilioni moja, lakini wilaya kama ya Mkalama imetengewa sh milioni 100 tu. Huu upendeleo huu, ni hatari sana na waziri atupe majibu.
“Maelezo yaje kwanini mikoa yenye hali mbaya ya maji inapata fedha kidogo kabisa, na ile yenye nafuu, inapata fedha nyingi, lakini mikoa yenye mawaziri ina bajeti kubwa zaidi,” alisema Lissu.
Naye Mbunge wa Mbozi Magharibi, David Silinde (CHADEMA), alisema maeneo wanayotoka mawaziri na manaibu wao wamekuwa wakijitengea fedha nyingi za miradi ili kuyanufaisha.
Alisema wakazi wa Wilaya ya Momba ni wengi, lakini fedha zilizotengwa kwenye miradi ya maji ni kidogo zaidi kuliko Mwanga anakotokea Waziri Maghembe, ambako kuna watu wachache zaidi.
Naye Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), ameibana serikali itoe kauli juu ya chanzo cha kifo cha Meneja Biashara wa Petroli wa Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), Julius Gashaza.
Mnyika alisema Gashaza,  aliripotiwa kujiua akiwa hotelini jijini Dar es Salaam baada ya kutoka kuhojiwa na Kamati ya Bunge.
“Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile wizara hii inahusika na EWURA, waziri atakapokuja kutoa majibu, aeleze chanzo cha kifo hicho,” alisema Mnyika.
Akitoa maoni kuhusu Bajeti ya Wizara ya Maji, Mnyika alisema njia bora ya kumsaidia Waziri Maghembe ni kuikataa bajeti ya mwaka huu wa fedha ili serikali ikajipange upya.
Alisema kila mbunge aliyechangia hoja kwenye bajeti ya wizara hiyo, anakiri imetengewa fedha kidogo, lakini mwisho wa siku anamalizia kwa kuiunga mkono.
Mnyika alisema Waziri Maghembe anaitwa mzigo, lakini hawezi kufanya vizuri kama fedha zinazoidhinishwa na wabunge, zitaendelea kutolewa kidogo.

No comments: