Monday 2 June 2014

Mtoto aliyefichwa ndani ya boksi kwa miaka 3 afariki dunia kwa kulaani

Mtoto aliyekuwa amefichwa kwenye boksi kwa miaka mitatu mfululizo Morogoro,Nasra Rashid (4),akiwa kwenye Wodi B ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbili(MNH)alikohamishiwa kwa matibabu zaidi
 
Mtoto Nasra Rashid Mvungi (4), aliyefichwa kwenye boksi kwa miaka minne, amefariki dunia katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na katika saa zake za mwisho za uhai wake alisikika akitamka maneno “sitaki waje kunichukua”.
Nasra ambaye alikuwa akitibiwa MNH, alifariki dunia usiku wa kuamkia jana baada ya hali yake kubadilika Alhamisi iliyopita, kiasi cha kuhamishiwa katika chumba cha uangalizi maalumu (ICU) ambako aliwekewa mashine ya kumsaidia kupata hewa ya oksijeni.
Mama mlezi wa Nasra, Josephine Joel alisema kabla hajawa mahututi, mtoto huyo alikuwa akiweweseka kwa kuzungumza maneno mengi hali iliyosababisha wauguzi kumfanyia ibada maalumu.
“Sitaki waje kunichukua, sitaki, sitaki, wasije kunichukua, bibi Nasra umesikia,” ni maneno aliyokariri mlezi huyo ambayo yalikuwa yakirudiwarudiwa na Nasra saa chache kabla ya hajawa mahututi na kupelekwa ICU.
Josephine alisema mtoto huyo pia kila mara alikuwa akidai apewe chips na soda na kwamba hadi mauti yalipomkuta alikuwa akitibiwa maradhi ya homa ya mapafu ‘nemonia’.
“Nasra alifariki saa 7.30 usiku, tangu Alhamisi iliyopita hali yake ilibadilika na kuwa mbaya na imeendelea kuwa hivyo hadi alipofariki dunia,” alisema na kuongeza:
“Bado niko Muhimbili nawasubiri watu wa ustawi wa Jamii kutoka Morogoro wao ndiyo watakuwa na uamuzi kuhusu mazishi ya mtoto huyo,” alisema.
Ofisa Habari wa MNH, Aminiel Eligaeshi alithibitisha kifo cha mtoto huyo, ambaye alipokewa hospitalini hapo Mei 26 mwaka huu akitokea Morogoro na kwamba hali yake ilibadilika ghafla juzi saa 2:00 usiku.
“Jitihada za madaktari zilifikia kikomo saa 7:30 usiku, baada ya mtoto huyo kupoteza maisha,” alisema.
Kuzikwa kishujaa
Ofisa ustawi wa jamii Mkoa wa Morogoro, Oswin Ngungatuti alisema mwili wa mtoto huyo utasafirishwa leo kwenda Morogoro.
Ngungamtitu alisema mazishi ya Nasra yatatanguliwa na ibada itakayoambatana na utoaji wa heshima za mwisho katika Uwanja wa Jamhuri, hatua ambayo alisema inatokana na baba mzazi wa mtoto huyo, Rashid Mvungi kuwa mmoja wa watuhumiwa wa mateso yake.

No comments: