Sunday 8 June 2014

Ufaransa watangaza kutoa wanajeshi wake jamhuri ya kati

Kutangazwa muda wa kuondoka majeshi ya Ufaransa huko CARJenerali Fransisco Soriano Kamanda wa majeshi ya Ufaransa katika Jamhuri ya Afrika ya Kati amesisitiza kwamba majeshi ya nchi hiyo yataanza kuondoka nchini humo tarehe 15 Septemba mwaka huu. Majeshi ya Ufaransa yalipelekwa Jamhuri ya Afrika ya Kati mwezi Disemba mwaka jana baada ya kushadidi mapigano Bangui, mji mkuu wa nchi hiyo ya Kiafrika. Rais Francois Hollande wa Ufaransa alidai kuwa, operesheni hiyo ilifanyika kwa lengo la kuisaidia serikali ya Bangui na kulinda maisha ya raia wa nchi hiyo. Hivi sasa nchi hiyo ya Magharibi imetangaza azma ya kuondoa majeshi yake nchini humo, baada ya kuyapeleka huko miezi sita iliyopita. Inafaa kuashiria hapa kuwa, mwezi Aprili mwaka huu, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio jipya baada ya hali ya kibinadamu kuwa mbaya nchini humo na hasa wimbi la mauaji yaliyofanywa na kundi la wanamgambo wa Kikristo la Anti Balaka dhidi ya Waislamu wa nchi hiyo. Kwa mujibu wa azimio hilo, iwapo jamii ya kimataifa haitatoa radiamali ya haraka kuhusiana na hali mbaya ya Jamhuri ya Afrika ya Kati, kuanzia tarehe 15 Septemba mwaka huu, kitapelekwa mjini Bangui kikosi cha wanajeshi wa kulinda amani wapatao  elfu kumi na askari polisi elfu moja mia nane. Ban Ki moon Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na mashirika ya kutetea haki za binadamu mara kadhaa yametahadharisha juu ya uwezekano wa kutokea janga la kibinadamu nchini humo. Umoja wa Mataifa mapema mwaka huu uliunda kamati iliyokuwa na jukumu la kuchunguza kwa kina chanzo cha mauaji, unyama na ukatili uliofanyika nchini humo.  Uchunguzi huo utaweza kuweka bayana iwapo kile kilichofanywa na wanamgambo wa muungano wa Seleka na wale wa Kikristo wa Anti Balaka, ni jinai za kivita na dhidi ya binadamu au la. Baraza la Usalama lilitahadharisha kwamba mashambulio ya kulipiza kisasi kati ya Waislamu na Wakristo mjini Bangui, ni mwanzo wa kuibuka vita vya pande zote, mauaji ya kimbari na kikabila nchini humo. Naye Bwana Mull Sebujja Katende mwakilishi  wa Uganda ambapo nchi yake ni  mwenyekiti wa mzunguko wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika amesisitiza kwamba moja ya vifungu vya baraza hilo ni kutiwa mbaroni na kufunguliwa mashtaka wale wote waliotenda jinai  kwenye nchi mbalimbali za Kiafrika. Hivi sasa kuna makubaliano kati ya Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa juu ya ulazima wa kufanyiwa uchunguzi wa kina matukio yote ya mauaji yanayofanyika barani humo. Pamoja na hayo yote, hatua ya Ufaransa ya kupeleka wanajeshi wake wasiopungua 2,000 huko Jamhuri ya Afrika ya Kati haikuweza kusaidia kurejesha amani na utulivu nchini humo, bali ilichangia kwa kiasi kikubwa  mwendelezo wa mauaji ya kundi la Anti Balaka dhidi ya Waislamu.

No comments: