Thursday 12 June 2014

Vita dhidi ya polisi na machinga ya peleka kilio jiji la mwanza

Zogo MwanzaWATU kadhaa wamejeruhiwa na baadhi ya magari yameharibiwa baada ya kuzuka kwa mapambano makali baina ya polisi na wafanyabiashara ndogondogo, maarufu kama machinga.
Mapambano hayo yaliyochukua zaidi ya saa sita, yalilifanya Jiji la Mwanza kutikisika kwa mabomu ya machozi na kugeuka uwanja wa mapambano yaliyosababisha kufungwa kwa maduka, ofisi na kusimamisha shughuli za kibiashara katika maeneo mbalimbali ya jiji kwa siku nzima ya jana.
Mmoja wa majeruhi aliyetambulika kwa jina la Fatuma Said, mkazi wa Nyamanoro, alikimbizwa katika Hospitali ya Mkoa ya Sekou Toure baada ya kugongwa na gari akiwa katika harakati za kukimbia vurugu hizo.
Mapambano hayo yalitokana na kitendo cha polisi pamoja na askari mgambo wa jiji kubomoa vibanda vya biashara vya wamachinga katika eneo maarufu la Makoroboi, katika kile kilichoelezwa kuwa ni kusafisha jiji.
Habari ambazo gazeti hili limezipata, zilisema kuwa wamachinga walichukizwa na kitendo cha polisi na mgambo wa jiji kubomoa vibanda vyao usiku wakiwa wamelala, na hivyo kushindwa kuokoa mali zao zenye thamani ya mamilioni ya fedha zilizokuwa ndani ya vibanda vyao.
Akizungumza kwa uchungu huku akilia, mmoja wa wamachinga hao aliliambia Tanzania Daima kuwa mali zao zenye thamani kubwa zimeteketezwa na kuharibiwa vibaya na askari hao, ambao hawakuwaruhusu kuchukua kitu chochote kutoka katika vibanda vyao.
“Kaka, wametuua, wamevunja mabanda yetu, wameharibu kabisa mali zetu na wamekataa katakata kuturuhusu kuokoa mali zetu.
“Wamevizia tumelala ndipo wakaja kufanya uharibifu huu. Kama wana haki kwanini wasije mchana, wakaacha tukaondoa mali zetu na wao wakaendelea na shughuli zao?” alisema machinga huyo ambaye hakuwa tayari kutaja jina lake.
Imedaiwa kuwa wafanyabiashara hao walizuiwa kuokoa mali zao hata baada ya kufika mapema eneo la Makoroboi, huku askari wa Jeshi la Polisi na wale wa mgambo wakiweka ulinzi mkali kila kona ya kuingia ndani ya soko hilo.
Hatua hiyo iliamsha hasira za wafanyabiashara hao ambao waliungwa mkono na wenzao kutoka sehemu nyingine pamoja na raia waliokuwa wakilaani hatua ya serikali kutumia nguvu kubwa za dola kupambana na raia wasiokuwa na hatia.
Inadaiwa kuwa wafanyabiashara hao waliamua kujikusanya kwa nia ya kuandamana kuelekea katika ofisi za Mkurugenzi wa Jiji, Hassan  Hida, kitendo kilichotafsiriwa na polisi kama maandalizi ya mashambulizi, hivyo kuanzisha mapambano.
Mali zinazodaiwa kuharibiwa za wafanyabiashara hao wanaokadiriwa kufikia 800 waliokuwa wanamiliki mabanda yao mbele ya nyumba za Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), ni pamoja na nguo, viatu, radio, vifaa vya umeme, mabegi, vifaa vya ujenzi na televisheni.
Watu 10 washikiliwa
Akizungumza na waandishi wa habari,Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Christopher Fuime,  alisema polisi inawashikilia watu kumi kwa tuhuma za kusababisha uvunjifu wa amani, licha ya kukana kuwepo kwa majeruhi kwa raia ama askari polisi.
Alisema wafanyabiashara hao wanaendesha shughuli zao kimakosa na kwamba eneo hilo limewekwa kwa ajili ya matumizi ya ziada.
“Kufanya zoezi hilo ni kuhakikisha mji wa Mwanza unakuwa na njia za wazi na kuweka jiji katika mazingira yaliyo salama na kuhakikisha kila mkazi anafuata sheria.
“Zoezi hili wananchi wanalifahamu kwa kuwa sio mara ya kwanza. Kuna makundi yanayosababisha hizi vurugu na tumeyashughulikia,” alisema.
Kauli ya wananchi
Wananchi waliokumbwa na mkasa huo, wameliambia waandishi wa habari kuwa ubomoaji huo sio wa haki na huenda kuna shinikizo la watu fulani wanaotaka kumiliki eneo hilo kutokana na unyeti wake.
Mbele ya waandishi wa habari, mmoja wa wananchi waliodhurika katika vurugu hizo, Joseph Mgaya, alisema kitendo cha polisi kurusha mabomu na kupiga watu ovyo, ni cha kinyama.
Serikali yatoa kauli bungeni
Wakati Jiji la Mwanza likiwaka moto, mjini Dodoma, serikali imeshindwa kutoa agizo la kusitiza operesheni safisha jiji hilo iliyosababisha machafuko hayo.
Hoja kuitaka serikali isitishe operesheni hiyo ilitolewa jana na Mbunge wa Nyamagana, Hezekie Wenje  (CHADEMA), wakati akitoa taarifa ya vurugu hizo bungeni.
“Hoja niliyonayo ni kwamba muda huu tulivyokaa hapa bungeni, mji wa Mwanza umechafuka, mabomu yanapigwa kila sehemu, maduka yote yamefungwa katika operesheni ya kuondoa wamachinga.
“Mheshimiwa Spika, operesheni ya aina hii, mwaka 2011 ilipofanyika kwa kutumia polisi, kuna maisha ya watu yalipotea Mwanza, mwaka 2012 operesheni kama hii ilitokea na kuna watu walipata ulemavu wa kudumu mpaka leo, na tambua kwamba suala la machinga ni la kitaifa, hivyo naiomba serikali kutoa kauli ya kusitisha operesheni hiyo,” alisema Wenje.
Akijibu hoja hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisema serikali inatafuta ukweli wa hali halisi, na hivi sasa Waziri Mkuu anaendelea na mazungumzo kushughulikia suala hilo ili liweze kumalizika.
“Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoka kwenda kuzungumza na wahusika, amekuja tu kupiga kura, tutachukua hatua kwa hili la Mwanza, lakini hatuwezi kulitolea kauli hapa ya kusitisha operesheni hiyo, ila tunaendelea kufanyia kazi na tutalitolea taarifa mara itakapokamilika,” alisema Lukuvi.

No comments: