Monday 2 June 2014

Mlipuko mwingine watokea Nigeria

Polisi Kaskazini mashariki mwa Nigeria wanasema kuwa shambulizi la bomu limewauwa zaidi ya watu 14 na kuwajeruhi wengine wengi.
Ripoti zimesema kuwa mlipuko huo uliotokea katika mji wa Mubi, ulilenga chumba kimoja cha burudani ambako watu walikuwa wakitazama mechi ya soka kwenye televisheni.
Katika miezi michache iliyopita, Boko Haram wamezidisha mashambulio yao hasa kaskazini mashariki mwa Nigeria. Mamia ya watu wameuawa na wengine wengi kujieruhiwa.
Pia wameshambulia nyumba za watu na kuzichoma moto, na kisa kilicho tikisa jamii ya kimataifa ni wasichana zaidi ya 200 waliotekwa nyara yapata miezi miwili sasa hadi leo hawajulikani waliko.
'Uharibifu uliozidi'
Mashambulio haya yameacha uharibifu mkubwa. Waliosalimika wamelazimika kukimbia makwao huku shule zikiachwa bila wanafunzi.
Uharibifu mkubwa wa mashambulio
Shambulio hilo limetokea karibu na mpaka kati ya Nigeria na Cameroon katika jimbo la Adamawa-mojawepo ya majimbo ambako sheria ya hali ya hatari inatumika kutokana na mashambulizi ya kundi la waislamu wenye itikadi kali la Boko Haramu.
Katika mwezi mmoja pekee watu zaidi ya 200 wameuawa katika mji huo.
Lakini sasa katika maeneo mengine ya kaskazini ambako inasemekana usalama umerejea kiasi, kama vile mji wa Kano juhudi zinafanywa kung'oa mizizi ya uovu huo.
Wanamgambo wa kiislamu AL shabaab wanaodaiwa kuwa na uhusiano na AL qaeda wamekuwa wakiwazuia wananchi kushiriki mambo yanayohusishwa na Mataifa ya magharibi. Inakisiwa kuwa zaidi ya wanafunzi milioni 11 kaskazini mwa Nigeria hawapewi mafunzo mengine yoyote mbali na ya kidini.
'Wanafunzi waathirika'
Mashirika ya kijamii hasa kutoka Uingereza yamekuwa yakifadhili kupitia taasisi za nchini humo masomo ya ziada hasa katika shule za mafunzo ya kidini, ili yatoe elimu ya ziada mbali na Qurani.
Tayari maelfu ya wanafunzi wanafaidi lakini bado kuna wengi zaidi wanaotishiwa usalama wao na inadaiwa ni kiasi kikubwa zaidi ya nchi hiyo haiwezi kufikiwa.
Licha ya mauaji ya miaka mingi yaliyofanywa na kundi hilo la Boko Haram na hata kujitangaza hadharani uhusiano wao na kundi la AL Qaeda, ni wiki iliyopita tu ambapo Umoja wa Mataiifa umeilitangaza kuwa kundi la kigaidi.
Japo wengi wanaona kuwa hatua hiyo imechelewa, bado inatoa matumaini ya kuweza kuchukuliwa hatua zaidi kusaidia kukabiliana na kundi hilo

No comments: