Thursday 30 July 2015

Azam yaigaragaza Yanga kwa mikwaju ya penati

AZAM FC jana ilimaliza ubabe wa Yanga katika michuano ya Kombe la Kagame baada ya kuibuka na ushindi wa penalti 5-4 katika mchezo wa robo fainali uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.
Timu hizo zilifikia hatua ya kupigiana penalti baada ya kutoka suluhu katika dakika 90 za kawaida za mchezo huo, uliokuwa wa vuta nikuvute katika kipindi chote.
Haji Mwinyi ndiye aliyeitia Yanga doa baada ya kukosa penalti ya tatu, huku Azam FC ikipata penalti zote tano. Waliofunga kwa upande wa Azam FC ni Kipre Tchetche, John Bocco, Humid Mao, Pascal Wawa na Aggrey Morris wakati walioifungia Yanga ni Salum Telela, Nadir Haroub na Godfrey Mwashiuya.
Haroub alikosa penalti katika mchezo dhidi ya Gor Mahia ya Kenya wakati Yanga ikilala 2-1, huku Simon Msuva na Amis Tambwe wakikosa penalti zao katika mchezo dhidi ya Telecom ya Djibouti, licha ya timu yao kuibuka na ushindi wa mabao 3-0 katika hatua ya makundi.
Kwa ushindi huo, Azam FC sasa watakutana na KCCA katika mchezo wa nusu fainali utakaofanyika kwenye Uwanja wa Taifa kesho, huku Gor Mahia ikicheza dhidi ya Khartoum ya Sudan katika mchezo utakaotangulia wa nusu fainali.

Ushindi huo wa Azam ni sawa na kulipa kisasi cha mwaka 2012 wakati Yanga ilipoibuka na ushindi wa mabao 2-0 katika fainali ya mashindano hayo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Yanga kwa muda mrefu imekuwa ikiisumbua Azam, ambapo mara ya mwisho waliifunga katika mchezo wa Ngao ya Jamii Agosti mwaka jana baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-0. Katika Ligi Kuu msimu uliopita, timu hizo hazikutambiana ambapo katika mechi ya kwanza zilifungana 2-2 na mechi ya pili zilifungana 1-1.
Katika mchezo wa jana,Azam FC ndio ilikuwa ya kwanza kufanya shambulizi kwa wapinzani wao mwanzoni kabisa mwa mchezo kupitia kwa John Bocco, lakini Mbuyi Twite aliondosha mpira huo katika hatari.
Dakika ya nne, Farid Mussa alijaribu kuwatoka mabeki wa Yanga na kupiga krosi iliyookolewa wakati Azam FC ikitawala sehemu kubwa ya dakika za mwanzo za mchezo huo. Juma Abdul nusura afunge katika dakika ya nane, lakini kipa wa Azam Aishi Manila aliokoa mchomo huo.
Shomari Kapombe wa Azam FC aliikosesha timu yake bao la kuongoza katika dakika ya 14, baada ya kushindwa kuunganisha wavuni krosi ya Mussa.
Juma Abdul wa Yanga alioneshwa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Farid Malik wa Azam FC, na Ame Ali wa Azam naye alioneshwa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Juma Abdul, ambaye alizimia na kutolewa uwanjani katika dakika ya 65 na nafasi yake kuchukuliwa na Joseph Zuttah.
Twite alioneshwa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Humid Mao. Azam FC walikosa bao la wazi katika dakika ya 85 baada ya Farid Malik kuwalamba chenga mabeki wa Yanga, lakini shuti alilopiga halikuwa na nguvu na kuokolewa na kipa Ally Mustapha.
Kocha Mkuu wa Yanga, Mholanzi Hans Van der Pluijm alisema baada ya mchezo huo kuwa, timu yake haikucheza vizuri katika kipindi cha kwanza lakini walijirekebisha kipindi cha pili katika mchezo huo uliokuwa na ushindani mkubwa.
Alisema ameridhika na kiwango cha uchezaji wa timu yake na wachezaji wake walifanya mazoezi ya kupiga penalti katika mazoezi na walifanya vizuri. Mwenzake wa Azam, Muingereza Stewart Hall alisema timu zote zilicheza vizuri na kila moja iliutawala mchezo kwa asilimi 50 lakini hakuridhika na uchezeshaji wa mwamuzi wa mchezo huo Davies Omweno wa Kenya.
Vikosi; Azam FC: Aishi Manila, John Bocco, Pascal Wawa, Aggrey Morris, Kipre Tchetche, Jean Mugiraneza, Farid Musa, Kheri Salum/Amme Ally, Humid Mao/Said Morad, Shomari Kapombe na Frank Domayo.
Yanga: Ally Mustapha, Nadir Haroub, Juma Abdul/Joseph Zuttah, Godfrey Mwaishuya, Donald Ngoma, Kelvin Yondani, Mbuyi Twite, Deus Kaseke/Salum Telela, Amissi Tambwe, Haruna Niyonzima/Malimi Busungu na Hajji Mwinyi.
Katika mchezo mwingine wa robo fainali uliochezwa awali, KCCA ya Uganda imetinga nusu fainali baada ya kuichapa mabao 3-0 Al Shandy ya Sudan kwenye uwanja huo wa Taifa.
KCCA inayofundishwa na Mike Muteebi, sasa inaungana na Gor Mahia ya Kenya na Khartoum N ya Sudan zilizotinga nusu fainali juzi. Gor Mahia iliifunga 2-1 Malakia ya Sudan Kusini wakati Khartoum iliichapa APR ya Rwanda mabao 4-0.
Mabao ya KCCA yalifungwa na Joseph Ochaya, Farooque Motovu na Thom Masiko

No comments: