Friday 24 July 2015

January Makamba afunguka baada ya kukatwa Jina lake

ALIYEKUWA mgombea urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) January Makamba, amefunguka na kuwataka wananchi wasife moyo kwa yeye kuishia nafasi ya tano kwa vile muda bado upo na kwamba hivi sasa wafanye kampeni za kufa mtu ili John Magufuli aliyechaguliwa na chama hicho aweze kushinda na kuingia Ikulu.

Akizungumza kwenye mkutano maalum wa Umoja wa Wanawake wa CCM wilayani hapa, ulioitishwa kwa ajili ya kuchagua madiwani wa viti maalum, Makamba aliyeomba tena kuchaguliwa kuwa mbunge katika jimbo la Bumbuli, alisema kwamba anawashukuru wote waliokuwa wakimuunga mkono hadi kufikia nafasi hiyo ambayo haikuwa yake, bali ni ya wananchi wa Lushoto waliomlea na Watanzania wote."Mafanikio niliyoyapata ya kuingia tano bora si yangu peke yangu ni fahari ya nyie wazazi wangu, msife moyo wakati bado upo lakini kwa sasa lazima tuhakikishe ndugu John Pombe Magufuli anakipatia chama chetu ushindi na kuingia Ikulu," alisema Makamba na kushangiliwa na akina mama hao.

Katika mchakato wa urais kupitia chama hicho January aliingia hatua ya tano bora pamoja na Bernad Membe, Amina Salum Ali, Dkt. Asha Rose Migiro na Dkt. Magufuli aliyeshinda kutoka kundi la watu 38 waliorudisha fomu na kupitia michujo mbalimbali ya CCM.

Akizungumza katika mkutano huo Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM wilayani hapa (MNEC), Dkt. Najim Msenga, aliwataka wananchi wa wilaya hiyo kubadilika na kuwachagua viongozi wanaolingana na January ili kuhakikisha wilaya hiyo inakuwa bora kwa viongozi watakaojali maslahi ya wananchi na waondoe watu wanaofanya 'unafki' kwa wengine.

"Ondoeni zama za unafiki chagueni watu wanaofaa na ambao wanafanana na January ambaye hata Rais amemwamini na kumchagua kwenye tano bora wakati wa kinyang'anyiro cha urais...Lushoto lazima mbadilike msichague kwa mazoea, chagueni viongozi watakaotusaidia shida zetu," alisema Najim.

Dkt. Najim alisema kwamba yeye hakuweza kugombea nafasi ya ubunge kama ambavyo baadhi ya wengi walivyotarajia kutokana na kuridhika na nafasi aliyochaguliwa na hakutaka kuwa na tamaa ya kugombea ubunge ingawa amekuwa na sifa na uwezo wa kuwaletea maendeleo wananchi wa Lushoto, amezingatia nafasi yake ambayo anataka kuonesha uwezo katika kuwatumia kichama.

"Mimi MNEC wenu nina sifa za kugombea ubunge lakini sikuchukua fomu jimbo lolote maana mmenipa nafasi hii bado sijawatumikia mkaona uwezo wangu, lakini nawaeleza hakikisheni mnachagua viongozi watakaoleta maendeleo yetu msichague mizigo," alisema Dkt. Najim.

Awali Katibu wa CCM wa wilaya Ramadhani Mahanyu na Katibu wa CCM mkoani Tanga, walipopata nafasi ya kuwasalimia wajumbe wa mkutano huo, walimsifia Makamba kwamba kitendo cha kuingia tano bora katika mbio za urais ni cha kujivunia wilaya hiyo na mkoa kwa ujumla lakini pia kimeonesha kijana huyo ni azina kwa chama hicho katika siku za usoni

No comments: