Sunday 26 July 2015

Rais Kikwete ateua Mkurugenzi mpya wa Uchaguzi

Rais Jakaya Kikwete akimwapisha Mkurugenzi wa Uchaguzi, Kailima Ramadhani Kombwey (kulia) Ikulu Dar es Salaam jana. Mwingine ni Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue
RAIS Jakaya Kikwete amefanya mabadiliko ya utendaji katika Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kwa kumteua aliyekuwa Mkurugenzi wa Utawala wa Tume hiyo, Kailima Kombwey kuwa Mkurugenzi wa Uchaguzi.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, Kombwey ambaye aliapishwa jana jioni, anachukua nafasi ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Uchaguzi, Julius Mallaba, ambaye ameteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Rais Kikwete pia amemteua Jaji Richard Mziray, kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na majaji wengine wapya 13 wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Taarifa hiyo pia imesema kuwa Jaji Mziray ambaye ameteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, kwa sasa ni Jaji wa Mahakama Kuu, Dar es Salaam. Majaji wengine wa Mahakama Kuu walioteuliwa na Rais Kikwete ni Ignas Kitusi ambaye ni Msajili Mkuu Mahakama ya Tanzania na Wilfred Dyansobera, ambaye ni Naibu Msajili, Mahakama Kuu.
Wengine ni Lameck Mlacha ambaye ni Naibu Msajili na Mwenyekiti wa Baraza la Rufani la Kodi; Salima Chikoyo ambaye ni Naibu Msajili, Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi; Isaya Arufani ambaye ni Naibu Msajili na Katibu wa Jaji Mkuu wa Tanzania na Mallaba.
Pia yumo Adam Mambi ambaye ni Katibu Msaidizi Tume ya Kurekebisha Sheria; Sirilius Matupa ambaye kwa sasa ni Msaidizi wa Rais, Sheria, Ofisi ya Rais, Ikulu; Issa Maige ambaye ni Wakili wa Kujitegemea na Licia Kairo ambaye ni Wakili wa Kujitegemea.
Dk Masoud Shaaban Benhaji, Wakili wa Kujitegemea na Mhadhiri Mwandamizi, Chuo Kikuu Huria, Dar es Salaam pia ameteuliwa kuwa Jaji Mahakama Kuu. Wengine ni Victoria Makani ambaye ni Wakili wa Kujitegemea na Rehema Kerefu ambaye ni Mwanasheria wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

No comments: