Thursday 28 May 2015

Kampuni ya kuzuia ajali yaanzishwa Tanzania

Kutokana na wimbi la ajali za barabarani linalosababisha vifo vya mamia ya watu na maelfu kujeruhiwa,wananchi wametakiwa kutoa taarifa kwa vyombo vya usalama pindi wanapoona kanuni na sheria za barabarani zinakiukwa na madereva wazembe.
Wito huo umetolewa na mkuu wa kikosi cha usalama barabarani Mohamed Mpinga wakati wa uzinduzi wa kampeni mpya ya kuhamasisha usalama barabarani ijulikanayo zuia ajali sasa,toa taarifa mapema ambayo inafanywa na kituo cha ITV na Radio One kwa kushirikiana na Vodacom pamoja na jeshi la polisi, ambapo amesema matukio ya ajali yatapungua endapo madereva wote watazingatia kanuni na sheria za usalama barabarani.
Akizungumza katika uzinduzi huo uliofanyika kituo kikuu cha mabasi Ubungo jijini Dar es Salaam mkurugenzi wa Radio One Sterio Deogratius Rweyunga amesema lengo la kituo cha ITV na Radio One ni kuhakikisha madereva hasa wanaobeba abiria na kwenda masafa marefu wanakuwa makini wawapo barabarani na kutii sheria ili kunusuru maisha ya watu na kutaja namba za kutoa taarifa za mienendo mibaya ya madereva ambayo ni 0800757575.
Baadhi ya madereva wa mabasi ya mikoani wameeleza sababu kadhaa zinazochangia ajali za barabarani ikiwemo ubovu wa miundombinu pamoja na abiria wenyewe ambao wamekuwa wakiwachochea kuongeza mwendo kwa madai ya kucheleweshwa wanakokwenda huku wakitishia kuhama kampuni ya basi husika kutokana na dereva kwenda mwendo mdogo.

No comments: