Saturday 23 May 2015

Mama adaiwa kumuuza mwanaye kwa Sh70,000

Image result for mama auza mtotoMkazi mmoja wa Kijiji cha Nanja, Kata ya Lepruko, wilayani Monduli, anadaiwa kumuuza mtoto wake wa kumzaa kwa mtu mwingine kwa Sh70,000 kwa madai kuwa ana maisha magumu.
Katika tukio hilo la kushangaza, inadaiwa mwanamke huyo (jina linahifadhiwa) aliamua kumuuza mtoto huyo wa kiume mwenye umri wa miezi minane katikati ya Mei, mwaka huu akiwa ametoka naye mkoani Singida.
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Nanja, Time Samsoni akizungumza juzi mbele ya Mratibu wa Chama cha Wanawake Wanasheria Tanzania (Tawla) Tawi la Arusha, Francisca Gaspar alisema walijaribu kumshawishi akamchukue mtoto wake, lakini aligoma.
Mwenyekiti Samsoni alidai kuwa mtu aliyemnunua mtoto huyo anaishi katika Kijiji cha Longonito na ana wadhifa mkubwa kijijini hapo.
“Kwa kweli tulisikitishwa na kitendo hicho cha huyo mwanamke kumuuza mtoto wake kwa Sh 70,000 akisingizia maisha magumu na ameshindwa kumlea,” alisema Samsoni.
Alisema walimwita mwanamke huyo kwenye ofisi ya kitongoji na kumhoji sababu zilizomfanya amuuze mwanaye, lakini aliwaaambia kuwa hana uwezo wa kumhudumia.
Mratibu wa Tawla, Gaspar alisema watahakikisha wanafuatilia suala hilo ili lipatiwe mwafaka. “Lakini tumeambiwa kuwa mama huyo ametoroka baada ya kuhojiwa na viongozi wa hapa kijijini na hajulikani aliko mpaka sasa.”
Alisema katika kipindi hiki ambacho Tawla inaadhimisha miaka 25 tangu ianzishwe, wanatoa elimu ya sheria kwa wanawake wa eneo la Nanja na Meserani, hivyo jamii iwe inatoa taarifa kwao wanapoona matukio kama hayo.
Nina uhakika kuna matukio mengi yanatokea huku vijijini ila taarifa zinashindwa kufikishwa na endapo mngetuarifu mapema, tungeshirikiana na polisi huyo mama aliyemuuza mtoto wake angekamatwa kabla ya kutoroka,” alisema Gaspar.
Mkazi mmoja wa eneo hilo, James Lengitambi alipongeza hatua ya mwanamke huyo kumuuza mtoto wake kuliko angemtupa chooni au kwenye mfuko wa Rambo kama wanavyofanya wanawake wengine.
“Tumezoea kusikia kwenye vyombo vya habari kuwa baadhi ya wanawake wanawatupa chooni watoto wao au kuwatelekeza kwenye mifuko ya plastiki, ila huyu amemuuza hajamuua,” alisema Lengitambi

No comments: