Thursday, 1 May 2014

Barthez akaribia kutua simba

Dar es Salaam. ‘Nenda, rudi’ za kipa wa Yanga, Ally Mustapha ‘Barthez’ zinakaribia kutimia baada ya kipa huyo kuanza mazungumzo na Simba ili arejee tena Mtaa wa Msimbazi kuichezea klabu hiyo kwa mkataba wa miaka miwili.
Kipa huyo alishajiunga na Yanga mara mbili akitokea Simba na endapo atasaini mkataba atakuwa akirejea kwa mara ya pili akitokea Jangwani.
Katibu mkuu wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema kocha wa timu hiyo, Zdravko Logarusic ndiye aliyependekeza Barthez asajiliwe ili kuongeza nguvu katika kikosi chao msimu ujao baada ya kuvutiwa na kiwango chake.
“Kocha ametaka msimu ujao awe na kikosi kisichozidi wachezaji 25, na katika mapendekezo yake alisema lazima Barthez asajiliwe, na tayari tumeshaanza mazungumzo na Barthez, huenda tukampa mkataba wa miaka miwili,” alisema Kamwaga.
Barthez ambaye amekuwa na wakati mgumu wa kupata nafasi kwenye kikosi cha Yanga hivi sasa, imeelezwa kuwa ameshaafikiana na Yanga kuwa anamalizia mkataba wake kisha atatua Simba, ambao amezungumza nao na tayari wamekubaliana asaini mkataba wa miaka mwili.
Mlinda mlango huyo ambaye pia alishawahi kuichezea Simba na kusoteshwa benchi kwa miaka mitatu na Juma Kaseja kabla ya kutimkia Yanga na kupanda chati kuwa kipa tegemeo ndani ya klabu hiyo, alijikuta kwenye wakati mgumu baada ya kufungwa mabao matatu katika mechi ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Simba iliyomalizika kwa sare ya mabao 3-3.

No comments: