Tuesday 2 June 2015

Mwanafunzi toka mzumbe nae atangaza nia ya kugombea Urais

Hamasa ya wanaCCM kutangaza nia ya kuwania urais imemwibua mwanafunzi Shahada ya Uzamili ya Utawala wa Umma katika Chuo Kikuu cha Mzumbe, Maliki Malupu (34).
Malupu alitangaza nia ya kugombea urais kupitia CCM akiahidi kushughulikia suala la elimu, afya, kilimo na michezo huku akijua kuwa umri wake haujatimia miaka 40 inayotakiwa kikatiba.
Akitangaza nia hiyo mjini Morogoro jana, Malupu alisema kutokana na uaminifu na uadilifu wake, ameamua kuwania nafasi hiyo pamoja na mambo mengine kwa kuwa ni haki yake kikatiba.
Alipoulizwa atatimizaje nia yake hiyo bila kuwa na sifa kikatiba, alisema vifungu vya katiba vinavyotaja umri vina utata, hivyo ameamua kuingia kuvitafutia suluhisho.
“Unajua ibara ya 39 (1) (b) inasema lazima utimize miaka 40, lakini ibara (d) inasema mtu mwenye sifa za kuwa mbunge au mjumbe wa baraza la wawakilishi anaweza kuwania urais,” alisema akifafanua kuwa yeye ana sifa hizo.
Akieleza sababu nyingine zilizomsukuma kuwania urais, Malupu alisema kuwa ni kuhakikisha sekta ya elimu inaboreshwa kikamilifu kwa kuwa muda mrefu imekuwa ikichezewa na baadhi ya viongozi.
Alisema muundo wa sekta hiyo unapaswa kurekebishwa kwa ama kufutwa au kuondoshwa utaratibu wa kupanga viwango vya ufaulu wa GPA kwa wanafunzi wa elimu ya sekondari katika mitihani ya kidato cha sita na cha nne.
Alisema utaratibu huo haufai kwa kuwa hautoi matokeo ya kuboresha maarifa kwa wanafunzi, pia unawaathiri wanafunzi kisaikolojia katika kujitofautisha wao na wanafunzi wa elimu ya juu.
“Nitahakikisha naboresha mitalaa kwa masomo ya kidato cha nne na cha sita ili kuleta weledi wa kina na wa kutosha, nitaboresha mazingira ya watumishi sekta ya elimu ikiwa ni pamoja na kuboresha mishahara na stahiki za walimu wa msingi hadi vyuo,” alisema.
Katika mkutano wake wa saa 1.30, Malupu alisema atahakikisha anadhibiti suala la maprofesa kuacha kazi yao ya weledi na kukimbilia katika siasa na ataboresha stahiki zao na mishahara kwa kuwalipa vizuri wanaofundisha vyuo vya Serikali na binafsi bila ubaguzi wowote ili kuimarisha sekta ya elimu ngazi vyuo vikuu.
Malupu alisema ataitazama sekta ya kilimo kwa kuongeza vyuo vikuu vya kilimo ili kuleta tija ya kilimo katika sekta hiyo na Serikali yake itakuwa na mkakati mahsusi wa kutoa elimu na mitaji kwa wakulima wanaofanya kilimo chenye tija na kilimo cha kujikimu. Katika afya, Malupu alisema kuwa atahakikisha suala la afya linasimamiwa kikamilifu ikiwa ni pamoja kuwapatia wazee huduma bure na kwamba zahanati, vituo vya afya na hospitali zinapatiwa vifaatiba vya kutosha ili kuondoa malalamiko kutoka kwa wananchi.
Malupu pia alizungumzia wananchi wanaoishi katika visiwa vya Ukerewe mkoani Mwanza na Mafia mkoani Pwani kuwa wamesahaulika, hivyo akiteuliwa na baadaye kuchaguliwa atahakikisha anakifanya kisiwa cha Ukerewe kuwa mkoa unaojitegemea ili kuwapunguzia wananchi umbali wa kufuata huduma Mwanza.

“Wananchi wa Visiwa vya Mafia na Ukerewe wanakabiliwa na changamoto za upatikanaji wa huduma za kimkoa kutokana na mazingira ya kijiografia na wamesahaulika kwa kiasi kikubwa,” alisema.
Katika hotuba yake hiyo, Malupu aliwataka vijana kutokata tamaa na kujitokeza kugombea nafasi za udiwani, ubunge na urais pamoja na kujiandikisha katika Daftari la Wapigakura na kujitokeza kutumia haki hiyo ya kikatiba kwa kupiga kura.
Michezo
Akizungumzia uboreshaji wa sekta ya michezo, Malupu alisema atahakikisha anaanzisha vituo vya kulea vipaji katika mpira wa miguu vitakavyowawezesha vijana kuibua vipaji na kuwapa elimu ya msingi kuhusu mpira wa miguu ili kuinua soka la Tanzania. Pia, aliahidi kuboresha sekta ya filamu na muziki kwa ujumla kwa kuwawekea vijana utaratibu maalumu ili waweze kujitengenezea ajira za kudumu.
Polisi na nyumba
Aliahidi kulipatia Jeshi la Polisi nyumba za shirika la nyumba ili kuondokana na wanazokaa ambazo hazilingani na hadhi walionayo... “Nia yangu ni kuhakikisha askari polisi wanakaa katika mazingira salama na yenye hadhi yao siyo kama ilivyo sasa,” alisema.

No comments: