Thursday 4 June 2015

Taifa starz yazindua jezi mpya

Hamasa na mapenzi makubwa waliyokuwa nayo Watanzania kwa timu yao ya Taifa, Taifa Stars yamepotea siku za karibuni kutokana na sababu mbalimbali, zikiwamo matokeo mabaya ya timu hiyo.
Hilo, limemfanya Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii, Said Mtanda afikirie kivingine na kutoa ushauri.
Jana, Mtanda aliyekuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya uzinduzi wa jezi mpya za Stars alitaka mashabiki na wadau wengine wa soka kurejesha mapenzi yao kwa Taifa Stars.
Uzinduzi huo uliofanyika jijini Dar es Salaam ulikwenda sanjari na utoaji vyeti kwa makundi mbalimbali ya watu, waliotoa mchango wao kwenye maendeleo ya mchezo wa soka nchini.
Katika uzinduzi huo, kulizunduliwa jezi aina tatu, ambazo ni jezi za ugenini, jezi za nyumbani na jezi zitakazokuwa zikitumika kwa ajili ya mazoezi.
Mtanda, ambaye ni Mbunge wa Mchinga mkoani Lindi alisema uzinduzi wa jezi hizo uwe chachu ya kurudisha hamasa na mvuto wa timu ya Taifa kwa Watanzania.
Alisema kuwa anaamini mabadiliko hayo ya jezi yatakwenda sanjari na hatua madhubuti za kuziimarisha timu mbalimbali za Taifa zifanye vizuri katika mashindano mbalimbali zitakayoshiriki.
“Kuna watu wanahoji hivi tunahitaji jezi mpya au timu yetu ya Taifa kufanya vizuri? Mimi naona tunahitaji vyote viwili. Tubadilishe namna ya kuendeleza timu yetu ya Taifa pia tubadilishe jezi zinazotumiwa Taifa Star,” alisema Mtanda.
Jezi hizo zitaanza kutumiwa na Stars kwenye maandalizi yao ya kufuzu fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon) na Michezo ya wachezaji wa ndani (Chan), zitakuwa ni nyeupe kwa mechi za ugenini, wakati kwa mechi za nyumbani zitakuwa za rangi ya bluu.
Akizungumza baada ya uzinduzi huo, kocha wa Taifa Stars, Mart Nooij alisema kuwa kikosi chake kiko tayari kwa ajili ya kupeperusha vyema bendera ya nchi katika mashindano yanayoikabili.
Nooij alisema kuwa kila mmoja kikosini anatambua deni ambalo timu hiyo inalo kutoka kwa mamilioni ya Watanzania, hivyo watapambana kuhakikisha wanaibuka na ushindi kwenye mechi hizo dhidi ya Misri na Uganda.
“Tunaendelea na maandalizi yetu na molali ya wachezaji iko juu. Wachezaji wanaendelea kuimarika siku hadi siku na kila mmoja wetu anajituma kwa kadri ya uwezo na majukumu yake ili tuwape furaha Watanzania,” alisema.
Nahodha wa timu hiyo, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ alisema kuwa mabadiliko hayo ya jezi yamewaongezea hamasa ya kuhakikisha wanaibuka na ushindi kwenye mashindano mablimbali ili kurudisha imani ya mashabiki kwa timu.
“Sisi, wachezaji tumeridhishwa na jezi mpya kwani zina rangi zote zilizopo kwenye bendera yetu ya Taifa, jambo ambalo linatuhamasisha kucheza kwa uzalendo zaidi,” alisema Cannavaro.
Stars inatarajia kuondoka nchini leo kwenda Addis Ababa, Ethiopia kwa maandalizi ya kuivaa Misri.
Katika hafla ya utoaji vyeti, baadhi ya makundi yaliyotunukiwa ni viongozi wa serikali, wanasoka wa zamani, timu ya Taifa iliyofuzu fainali za Mataifa ya Afrika, waamuzi na makocha mbalimbali wa soka.
Katika hatua nyingine, Rais wa TFF , Jamal Malinzi jana pia alizindua rasmi tovuti mpya ya TFF yenye anwani ya www.tff.or.tz.
Malinzi alisema: “Tumeamua kufanya jambo hili katika kuenzi miaka hamsini ya kujiunga na Fifa ili kutoa msisitizo kuwa sasa TFF na sisi tunajiunga na kuendeleza mpira kisasa kulingana na teknolojia iliyopo.
“Kupitia tovuti hii wadau wa mpira watapata fursa ya kuhabarishwa na kuelimishwa kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu mpira wa miguu.”
Aliongeza: “Tovuti hii itakuwa pia na sehemu ya kumbukumbu zihusuzo historia ya mpira wa miguu na matukio mbalimbali katika historia ya mpira wetu.”

No comments: