Thursday 8 May 2014

Uhalifu dhidi ya binadamu Sudan Kusini

Viongozi wa Sudan Kusini wanatarajiwa kukutana kwa ajili ya kurejesha amani nchini humo
Ripoti ya Umoja wa Mataifa kuhusu vita vya wenyewe kwa wenyewe vinavyoendelea nchini Sudan Kusini, imelaumu pande husika kwenye mgogoro huo kwa kutekeleza uhalifu dhidi ya binadamu.
Ripoti hiyo imeelezea kufanyika kwa mauaji ya watu wengi wasio na hatia kwa misingi ya ukabila.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, takriban waathiriwa 900 waliohojiwa , wamezungumzia ukatili waliotendewa na wanjeshi pamoja na waasi.
Ripoti hiyo imetuhumu wanjeshi wa serikali kwa kuwabaka wanawake na kuwakamata wengine ili kuwatumia kamawatumwa wa ngono.
Mapema leo, shirika la kimataifa la Amnesty International limetuhumu pande zote mbili zinazozozana katika mgogoro huo kwa kutenda uhalifu dhidi ya binadamu na vitendo vingine vibaya vya ukiukwaji wa haki za binadamu.
Shirika hilo linasema kuwa ushahidi wake umetokana na waathiriwa wenyewe kusimulia yaliyowakumba baada ya kushambuliwa kwa misingi ya ukabila huku wakitendewa dhuluma za kingono.
Ushahidi wa visa vya ubakaji, wizi na uchomaji wa miji na vijiji pia umeripotiwa.
Kwa mujibu wa shirika hilo, maelfu ya watu wameuawa wengi wakiwa katika nyumba zao au katika maeneo ya kuhifadhi wakimbizi.
Kulingana na taarifa za kina zilizokusanywa moja kwa moja kutoka kwa waathiriwa na mashahidi, Ripoti hiyo inasema kuwa maelfu ya wanaume, wanawake na watoto wameuwawa huku nyingi ya mashambulio yakichochewa kikabila.
Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir na kiongozi wa waasi Riek Machar wanapangiwa kukutana kwa mazungumzo ya amani hapo kesho ijumaa

No comments: